MASIKU
 Mbaraka Mwishehe ametiwa mbaroni na Jeshi la Polisi Kinondoni, Dar es 
Salaam kwa madai ya kuwashambulia kwa kisu watu wawili wa familia moja. Tukio
 hili lilitokea hivi karibuni Mwananyamala Kisiwani, Dar ambapo kwa 
mujibu wa taarifa ya kipolisi, mtuhumiwa huyo alikutwa ndani ya nyumba 
ya Nelson Ainea Shoo, saa kumi na moja alfajiri. Akizungumza na Amani, mke wa Nelson aliyejitambulisha kwa jina la Neema Hamis Zame (32), alikuwa na haya ya kusema:
“Siku ya tukio, ilikuwa alfajiri kabla hatujaamka, ghafla nilimsikia 
shemeji yangu aitwaye Goodluck (Ainea Shoo) akipiga kelele na kusema: 
‘Kaka kuna mwizi.’ Mume wangu aliamka akatoka kuelekea sebuleni na mimi 
nilikuwa nyuma yake. “Kufika, tulimkuta shemeji amelala sakafuni huku 
utumbo ukiwa nje na damu nyingi zikimtoka, alikuwa akikoroma, kumbe 
alichomwa kisu kwenye paja, mara mbili tumboni na begani. “Nilikimbilia 
chumbani kuchukua khanga na kumfunga ili kuzuia damu isitoke kwa wingi, 
pia utumbo usiendelee kumwagika huku mume wangu akimdhibiti yule 
mtu. “Cha ajabu, muda mfupi mume wangu naye akawa chini anatokwa damu, 
kumbe hata yeye alikuwa amechomwa kisu mara tatu tumboni na utumbo 
ukatoka nje.
“Hali ndani ilikuwa mbaya, sakafu ilitapakaa damu. Nikamwita shemeji 
yangu mwingine aitwaye Erick (Ainea Shoo), yeye akapambana na yule mtu 
wakati mimi nawahudumia wale majeruhi. “Nilipata akili za haraka, 
nilikwenda kumuita mlinzi akaingia na kushirikiana na shemeji 
wakamdhibiti. Huwezi kuamini, eti yule mtu akaomba asamehewe kwa vile 
hakujua kama alikuwa ameingia katika nyumba yetu.
“Hakuna aliyemsikiliza kwani alikuwa amefanya kosa kubwa, akaingizwa 
kwenye gari hadi polisi kuchukua PF3 na likafunguliwa jalada 
(OB/RB/20201/2013 Kujeruhi) kisha majeruhi tukawapeleka Hospitali ya 
Muhimbili. “Kilichotokea hospitali,  shemeji alitolewa bandama kwa vile 
iliharibika kutokana na majeraha ya kisu,” alisema Neema.
Naye baba mzazi wa majeruhi hao, mzee Ainea Shoo ambaye alitoka 
Machame Moshi, Kilimanjaro baada ya kupata taarifa hizo, alisema 
mtuhumiwa huyo alikuwa na dhamira ya kuwatoa roho watoto wake hao, 
akaliomba jeshi la polisi kushughulikia kesi hiyo kwa uwazi na 
kuhakikisha haki inatendeka. Mlinzi wa nyumba hiyo, Boli Mtumwa 
alipohojiwa na gazeti hili alikiri kutokea kwa tukio hilo na kusema yeye
 na mdogo wa Nelson ndiyo waliomdhibiti mtuhumiwa na kumpeleka 
polisi. Dada wa mtuhumiwa aliyejitambulisha kwa jina la Taji Mbaraka 
alikiri kukamatwa kwa kaka yake huyo lakini hakuwa tayari kuzungumza 
zaidi kwa sababu suala hilo lipo mkononi mwa dola. Kaimu Kamanda wa Mkoa
 wa Polisi Kinondoni, ACP Yusuf Mrefu alikiri kutokea kwa tukio hilo na 
kusema kuwa mtuhumiwa anaendelea kushikiliwa huku upelelezi ukiendelea. 
source: GPL

 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni