Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Sarah Dumba
Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Dk. Rehema Nchimbi, alisema jana kuwa Sarah
 alifariki dunia juzi saa moja jioni, katika Hospitali ya Wilaya ya 
Njombe ya Kibena, alikokuwa amepelekwa kwa matibabu.    
Alisema mkuu huyo wa wilaya aliugua ghafla juzi muda mfupi baada ya
 kutoka ofisini na alianza kujisikia vibaya alipokuwa akijiandaa kula 
chakula alichokuwa ameandaliwa.
“Mkuu wa wilaya alipofika nyumbani kwake, alitaka kupata chakula 
lakini alianza kupata shida ya kupumua na baadaye kuanza kulegea mwili. 
Alipelekwa katika Hospitali ya Kibena ndipo umauti ukamfika akipatiwa 
matibabu,” alisema Dk. Nchimbi
Dk. Nchimbi alisema mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali
 Teule ya Wilaya ya Wanging’ombe ya Ilembula, ambayo ndiyo ina uwezo wa 
kuhifadhi maiti.
Alisema mipango ya mazishi inaendelea kufanywa na kwamba leo 
kutakuwa na ibada maalum ya kuaga mwili wake katika Kanisa Kuu la 
Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kusini mjini hapa, 
alikokuwa akiabudu.
Mkuu wa Mkoa alisema baada ya hapo, mwili wa marehemu utasafirishwa
 kwenda Dar es Salaam, ambako familia yake inaishi maeneo ya Kigamboni, 
kwa maziko ambayo yatafanyika siku ya Alhamisi tarehe 24/3/2016. 
Sarah alianza kazi ya ukuu wa wilaya mwaka 2006 katika wilaya ya 
Kilindi mkoani Tangana baadaye kuhamia Njombe (wakati huo ikiwa katika 
mkoa wa Iringa) na sasa mkoa wa Njombe, alikotumika hadi kufariki dunia.
 
