WAFANYABIASHARA wawili, Harbinder Sethi na James Rugemalira 
wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es 
Salaam kwa mara ya pili na kusomewa mashitaka mapya sita likiwamo la 
utakatishaji fedha na kusababisha hasara ya Dola za Kimarekani milioni 
22.1 na Sh bilioni 309.4.
Rugemalira ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya VIP Engineering na 
mmiliki mwenza wa zamani wa Kampuni ya Kufua Umeme ya Independent Power 
Tanzania Ltd (IPTL) na Sethi ambaye ni Mwenyekiti Mtendaji wa Kampuni ya
 Power African Power (T) Limited (PAP), walisomewa mashitaka hayo jana 
mbele ya Hakimu Mkazi, Huruma Shaidi, yakifanya sasa wakabiliwe na 
mashitaka 12 baada ya awali kupandishwa kizimbani Juni 19, mwaka huu, 
ambako walikabiliwa na mashitaka sita.
Akiwasomea mashitaka hayo, Wakili wa Serikali, Shedrack Kimaro alidai
 washitakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka ya kula njama, kujihusisha na 
mtandao wa uhalifu, kughushi, kutoa nyaraka za kughushi, kujipatia fedha
 kwa njia za udanganyifu, kuisababishia serikali hasara na kutakatisha 
fedha. Kimaro alidai kati ya Oktoba 18, 2011 na Machi 19, 2014 jijini 
Dar es Salaam, walikula njama katika nchi za Afrika Kusini, Kenya na 
India ili kutenda kosa.
Alidai katika mashitaka ya pili kati ya Oktoba 8, 2011 na Machi 
19,2014 jijini Dar es Salaam, wakiwa siyo watumishi wa umma 
walishirikiana na watumishi wa umma kutekeleza mtandao huo wa uhalifu 
kwa lengo la kujipatia faida.
Katika mashitaka ya tatu yanayomkabili Sethi, inadaiwa kuwa Oktoba 
10, 2011 katika Mtaa wa Ohio Manispaa ya Ilala jijini Dar es Salaam 
akiwa na nia ya ulaghai, alighushi fomu namba 14 A ya usajili wa kampuni
 na kuonesha kuwa yeye ni Mtanzania anayeishi Kitalu namba 887 Mtaa wa 
Mrikau, Masaki wakati akijua sio kweli.
Pia Sethi anadaiwa alitoa nyaraka ya kughushi ambayo ni fomu namba 14
 A ya usajili wa kampuni kwa Ofisa Msajili wa Kampuni, Seka Kasera kwa 
njia ya kuonesha kwamba yeye ni Mtanzania na Mkazi wa Mtaa wa Mrikau, 
Masaki Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Aidha, Kimaro alidai katika mashitaka ya kujipatia fedha kwamba kati 
ya Novemba 28 na 29, 2011 na Januari 23,2014 katika Makao Makuu ya Benki
 ya Stanbic Kinondoni na Benki ya Mkombozi, Tawi la Mtakatifu Joseph, 
kwa ulaghai washitakiwa hao walijipatia kutoka Benki Kuu ya Tanzania 
(BOT), Dola za Marekani 22,198,544.60 na Shilingi za Tanzania 309, 
461,300,158.27.
Pia washitakiwa wote wanadaiwa kuisababishia serikali hasara ambapo 
inadaiwa walitenda makosa hayo Novemba 29, 2013 katika Benki ya Stanbic,
 Tawi la Kinondoni, kwa vitendo vyao waliisababishia serikali hasara ya 
Dola za Marekani 22, 198, 544.60 na Sh 309,461,300,158.27.
Kimaro alidai kati ya Novemba 29,2013 na Januari 23, 2014 maeneo 
tofauti Dar es Salaam, kwa pamoja walitenda kosa la kutakatisha fedha 
kwa kuchukua fedha kutoka BoT ambazo ni dola za Marekani milioni 22.1 na
 Sh bilioni 309.4 wakati wakijua fedha hizo ni zao la kujihusisha na 
genge la uhalifu.
Katika mashitaka ya nane, Kimaro alidai kuwa Novemba 29, 2013 katika 
Tawi la Benki ya Stanbic Tanzania, Wilaya ya Kinondoni, Sethi 
alitakatisha fedha kwa kuchukua kutoka BOT dola za Marekani milioni 22.1
 wakati akijua fedha hizo zimetokana na zao la kujihusisha na genge la 
uhalifu.
Aidha, Sethi anadaiwa kuwa kati ya Novemba 29, 2013 na Machi 14,2014 
katika Tawi la Benki ya Stanbic Kinondoni, Dar es Salaam alitakatisha 
fedha Sh bilioni 309.4 kutoka Benki Kuu ya Tanzania wakati akijua fedha 
hizo zimetokana na zao uhalifu.
Katika mashitaka ya 10, inadaiwa Januari 23, 2014 katika Benki ya 
Mkombozi, Tawi la St Joseph Cathedral, Rugemalira alitakatisha fedha 
ambazo ni Sh bilioni 73.5 kutoka kwa Sethi wakati akijua fedha hizo 
zimetokana na zao la kujihusisha na genge la uhalifu.
Pia inadaiwa Januari 23, 2014 katika tawi hilo la Benki ya Mkombozi, 
Rugemalira alitakatisha fedha ambazo ni dola za Marekani milioni 22 
kutoka kwa Sethi wakati akijua fedha hizo ni zao la uhalifu.
Kimaro pia alidai Sethi anadaiwa kuwa Januari 28, 2014 katika Tawi la
 Benki ya Stanbic, Kinondoni alihamisha Rand za Afrika Kusini 1,305,800 
kwenda kwenye akaunti namba 022655123 katika Benki ya Standard Land 
Rover Sandton ya Afrika Kusini wakati akijua katika kipindi anahamisha 
fedha hizo zimetokana na zao la kujihusha na genge la uhalifu.
Washtakiwa hao hawakutakiwa kujibu chochote kwa sababu mahakama hiyo 
haina mamlaka ya kusikiliza kesi za uhujumu uchumi. Hata hivyo, upande 
wa mashitaka ulidai kuwa upelelezi wa shauri hilo haujakamilika na 
washitakiwa wamerudishwa rumande hadi Julai 14, mwaka huu kwa kuwa 
mashitaka ya kutakatisha fedha yanayowakabili washtakiwa hao hayana 
dhamana.