
Na Mwandishi Wetu, Tabora
MKUU wa Wilaya ya Uyui mkoani Tabora, Gabriel Mnyele, amejiuzulu wadhifa wake, huku akiwa na siri nzito.
Mnyele ambaye kitaaluma ni mwanasheria msomi,  amejiuzulu jana huku 
akiwa amedumu katika wadhifa huo kwa miezi minane tangu ateuliwe na Rais
 Dk. John Magufuli. 
Hata hivyo hakuweka wazi sababu za kujiuzulu kwake.
Taarifa zinaeleza kuwa, jana Mnyele alikutana na Kamati ya Madiwani 
wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), na kuwaaga rasmi kuwa yeye si mtumishi 
tena wa Serikali.
Akizungumza na MTANZANIA jana, Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya 
hiyo, Said Ntahoni ambaye alihudhuria kikao cha madiwani wa Wilaya ya 
Uyui,  alikiri kujiuzulu kwa Mnyele na kusema ameacha pengo kubwa katika
 wilaya hiyo.
“Ni kweli amejiuzulu nafasi hii tangu jana, amekuja mbele ya Kamati 
ya Madiwani CCM Wilaya, akatwambia amejiuzulu nafasi yake, japo hakuweka
 wazi sababu za kuchukua uamuzi huo.
“Aliwaambia wajumbe kwamba amemwandikia barua Rais Magufuli na 
ameridhia aachie ngazi…wajumbe wengi walibaki wameduwaa kwa sababu yeye 
ndiye mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya yetu… kwa kuwa
 ni uamuzi wake hatukuwa na namna tena.
“Tumekuwa naye kwa miezi nane hapa, ametusaidia katika mambo mengi, 
nguvu yake ilikuwa bado inahitajika kwa wanaUyui ambao amekuwa akifanya 
nao kazi za kila siku,” alisema Ntahoni.
Alisema pengo la Mnyele ni kubwa, lakini anaamini Rais Magufuli 
atawapelekea kiongozi mwingine mchapakazi ambaye watashirikiana nae kwa 
kila nyanja ili kuinua maendeleo ya wilaya hiyo.
MNYELE
MTANZANIA ilimtafuta DC Mnyele na alipoulizwa iwapo amejiuzulu nafasi 
yake, alianza kwa kusema. “Ndo nasikia kwako niko ofisini kwangu 
naendelea kuchapa kazi niliyotumwa na mamlaka za uteuzi.
“…unajua unapoteuliwa unatangazwa, unapotumbuliwa unatangazwa sasa taarifa hizo wewe umezitoa wapi?
“Ukitaka kujua suala hili, sehemu nzuri na ‘source’ wa uhakika mtafute 
Gerson Msigwa (Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu), anajua ‘issue’ (suala) 
hili,” alisema Mnyele.
Hata hivyo Msigwa alipotafutwa kuzungumzia suala hilo, alisema 
hajapata taarifa zozote kutoka mamlaka zinazohusika juu ya kiongozi huyo
 kujiuzulu.
Wakati ikiwa haijulikani sababu za kujiuzulu kwake, taarifa nyingine 
zinasema Mnyele amefikia uamuzi huo kwa kile kinachodaiwa kuwa ni 
kutokana na kutingwa na majukumu yake binafsi aliyonayo.
Chanzo chetu cha uhakika, kinasema Mnyele aliandika barua ya kuomba 
kijiuzulu mwaka jana, kwa Rais Magufuli ambayo ombi lake limekubaliwa na
  amejibiwa juzi.
Baadhi ya watumishi wa halmashauri hiyo ambao hawakutaka kutajwa 
majina yao, waliiambia MTANZANIA kuwa jana asubuhi Mnyele alipita kila 
idara akianzia ofisini kwake kuaga wafanyakazi, huku akionekana kuwa ni 
mwenye furaha.
“Bosi wetu alianzia ofisini kwake kuaga watumishi, baadae alipita 
kila idara na kubwa ambalo alikuwa akieleza ni uamuzi ambao ameufanya 
yeye mwenyewe bila shinikizo.
“Bosi wetu kasema  uamuzi wa kusitisha ajira yake hautokani na 
kushindwa kwendana na kasi ya Rais Dk. Magufuli, bali anataka kufanya 
kazi zake
binafsi,” alisema mmoja wa watumishi wa halmashauri hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo (DED), Hadija Makuwani  
alisema yeye ni miongozi mwa watu walioagwa jana asubuhi na mkuu huyo wa
 wilaya.
Juhudi za kumpata  Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri ili kuzungumzia
 suala hilo, hazikufanikiwa kutokana na kuwa wilayani Nzega kwa shughuli
 ya ukaguzi wa maghala ya  kuhifadhia chakula.
CHANZO MTANZANIA