Muungano huo umesema umefikia uamuzi wa kusimamisha mashambulizi hayo ya
 anga ambayo yamekuwa yakiendelea kwa wiki nne sasa, baada ya kutimiza 
malengo yake ya kijeshi, ya kuondoa kitisho cha usalama wa Saudi Arabia 
na nchi nyingine majirani.
Umesema sasa unageukia mchakato wa kisiasa kujaribu kuusuluhisha mgogoro
 wa Yemen, na kuongeza kuwa uwezekano wa kuanza upya kwa mashambulizi 
hayo unaachwa wazi, ikiwa hali italazimu hivyo. Vile vile, kulingana na 
tangazo la muungano huo unaoongozwa na Saudi Arabia, mzingiri wa bahari 
na anga utaendelea dhidi ya Yemen, ambayo iko katika eneo la kimkakati 
katika Mashariki ya Kati.
Msemaji wa jeshi la Saudi Arabia Brigedia Jenerali Ahmed Asiri amesema 
uamuzi huo umefuatia ombi la rais wa Yemen. Abd-Rabo Mansour Hadi 
aliyeko ukimbizini nchini Saudi Arabia.
 
Msemaji wa jeshi la Saudi Arabia, Brigedia Jenerali Ahmed Asiri
 
Amesema, ''Leo uongozi wa muungano umeamua kusimamisha 
operesheni ''Dhoruba Kabambe'' kufuatia maombi ya rais wa Yemen, ambaye 
anaamini malengo makuu ya operesheni hiyo yametimia, kitisho kwa watu wa
 Yemen kimeondolewa, na waasi wa kihouthi wamepoteza uwezo wa kuwatisha 
watu wa Yemen na jirani zao. Serikali ya Yemen itachukua hatua 
kuwarejeshea matumaini watu wa nchi hiyo''.
Bado wahouthi wanashika hatamu
Hata hivyo licha ya madai hayo ya mafanikio, waasi wa kihouthi bado 
wanaudhibiti mjini mkuu wa Yemen, Sanaa, na rais Abd-Rabo Mansour Hadi 
bado yuko ukimbizini nchini Saudi Arabia. Hali kadhalika mapambano 
makali yanaendelea katika mji wa bandari wa Aden.
Iran, taifa la kishia ambalo linashutumiwa kuwaunga mkono wahouthi, 
imeukaribisha uamuzi huo wa kusitisha mashambulizi, ikisema ni hatua 
nzuri inayofungua mlango kwa njia za kisiasa kuusuluhisha mzozo wa 
Yemen.
Waziri wa mambo ya nje wa Iran Mohammad Javad Zarif amesema hatua hiyo 
haina budi kufuatiwa na msaada wa kibinadamu na mjadala miongoni mwa 
wayemen na serikali yenye kushirikisha makundi yetu. ''Tuko tayari 
kusaidia'', amesema waziri huyo kupitia ukurasa wake wa mtandao wa 
Twitter.
Marekani yapeleka meli za kivita
 
Marekani yajizatiti kuweza kuizuia Iran kupeleka silaha Yemen
 
Marekani pia imesema imelipokea vyema tangazo hilo la 
kusimamisha mashambulizi dhidi ya wahouthi, na kutoa rai ya kufanyika 
haraka mazungumzo ili kuepusha mvutano baina ya mataifa yenye ushawishi 
katika ukanda huo.
Hata hivyo Marekani imetuma meli yake ya kubeba ndege za kivita USS 
Theodore Roosevelt, ikisindikizwa na nyingine ya kubeba makombora USS 
Normandy, kukiwa na ripoti kwamba msafara wa meli tisa za Iran zimeng'oa
 nanga na kuanza safari baharini.
Msemaji wa wizara ya ulinzi ya Marekani Kanali Steven Warren amesema 
meli za Marekani zilikuwa zikijiandaa kuuzuia msafara huo wa Iran, ikiwa
 utakuwa umebeba silaha.
Waasi wa kihouthi wameitisha maandamano makubwa mjini Sanaa leo, 
kuadhimishwa kusitishwa kwa mashambulizi ya Saudi Arabia na washirka 
wake.
Mwandishi: Daniel Gakuba/afpe/rtre
Mhariri: Grace Patricia Kabogo